Friday, June 2, 2017

UCHAGUZI MKUU KENYA WAKWAMISHA BUNGE LA NNE LA EALA

Na JANETH MUSHI,

-ARUSHA

BUNGE la Nne la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA),lililopangwa kuanza Juni 5, Mwaka huu, huenda lifanyike kutokana na uchaguzi wa wabunge kutoka nchini Kenya kushindwa kufanyika kwa wakati.


Kauli hiyo ilitolewa juzi jijini Arusha jana na Spika wa Bunge hilo Daniel Kidega muda mfupi baada ya kulivunja bunge la tatu.

Akizungumza na waandishi wa habari Spika Kidega alisema mpaka sasa nchi tano wanachama zimeshakamilisha uchaguzi wa wabunge wa EALA na kusalia nchi moja ya Kenya.

Alizitaja nchi ambazo tayari zimeshakamilisha uchaguzi huo ni Tanzania, Uganda,Burundi,Rwanda na Sudani Kusini ambapo kila nchi imekamilisha uchaguzi wa wabunge tisa.

“Kenya pekee ndiyo hawajafanya uchaguzi mpaka sasa wa wawakilishi wao,jambo linaloweza kuchangia kukwama kuanza kwa Bunge la Nne, kwani lazima wawakilishi wa nchi zote wawepo ndipo bunge lianze,” alisema Spika Kidega aliyemaliza muda wake.

Alisema EALA imepanga kuwasiliana na Serikali ya Kenya ili kuomba uchaguzi huo ufanyike haraka hatua itakayowezesha vikao vya bunge hilo kwenda kwa wakati uliopangwa badala ya kuchelewa.

"Tunaomba Kenya iharakishe kufanya uchaguzi wa wawakilishi wao,hatutaki tatizo kama lililotokea kwenye Bunge la Pili baada ya kuchelewa kuanza kwa takribani miezi Sita. Kinachoonekana nchini Kenya ni uchaguzi wa wabunge EALA kuingiliana na uchaguzi Mkuu,"alisema Spika Kidega.

Akihitimisha mazungumzo yake nje ya ukumbi wa Bunge la EALA mjini hapa Spika Kidega aliwashukuru waandishi wa habari kwa namna walivyojitoa kuandika habari za bunge hilo vikiwamo vikao mbalimbali.

Aidha katika kikao hicho cha mwisho,Mbunge wa EALA kutoka Tanzania,Shyrose Bhanji,aliwasilisha  hoja binafsi iliyoungwa mkono na wabunge wengine, kuhusu maazimio ya kuwepo mtaala wa pamoja wa elimu katika Shule za Msingi na Sekondari za nchi wanachama wa Jumuiya hiyo.

Akiwasilisha hoja hiyo Shyrose alisema kuwa kuanzishwa kwa mtaala huo wa pamoja utaimarisha ushirikiano katika nchi wanachama na kuwa itaboresha masuala ya biashara,jamii na ustawi wa kiuchumi  kwa ujumla.

Alisema kuwa kuoanisha mitaala kutasaidia jamii kuwa na uelewa kuhusu jumuiya kwani asilimia 65 ya idadi ya  vijana waliopo katika nchi wanachama,wana uelewa kidogo kuhusu faida za ushirikiano na umoja wa Jumuiya hiyo hivyo kuna haja ya kuweka  mkakati wa kina ili kuendelea kutoa elimu kuhusu jumuiya ili vijana watambue fursa zilizopo.

Akichangia hoja hiyo Mbunge kutoka Rwanda,Martin Ngoga alisema kuwa hoja hiyo ni ya msingi na kuwa  hivi karibuni  nchini Rwanda kumeshapitishwa sheria kwamba  lugha ya kiswahili ianze kufundishwa mashuleni hivyo masomo kuhusu jumuiya yatakapoanza kufundishwa,itarahisisha kuwaweka wananchi karibu na kusaidia kusonga mbele.

"Hii ni hoja ya msingi kwani katika mkataba wa uanzishwaji wa jumuiya,mojawapo ya misingi muhimu sana ni kwamba tuwe na jumuiya ambayo imejengwa kwenye misingi ya kukubalika kwa watu wa jumuiya.Kwa hiyo ili tuwe na wananchi wanaoikubali jumuiya na ambao wako tayari kuitetea na kuilinda ni lazima tuanzie na vijana ambao ndiyo wengi,"alisema na kuongeza

"Somo kuhusu Jumuiya lina umuhimu wake na misingi yake na  likifundishwa kwa kiswahili itakuwa vizuri kama ambavyo tulipitisha azimio kwamba tufanye lugha ya Kiswahili kama lugha mojawapo rasmi ya Jumuiya,itarahisisha kuwaweka wananchi karibu,"


Mwisho

No comments:

Post a Comment