Sunday, June 11, 2017

POLISI WADAIWA KUFYATULIA MABOMU WACHIMBAJI WADOGO WA TANZANITE CHINI YA MGODI

Na MWANDISHI WETU
-SIMANJIRO   


ASKARI Polisi wilayani Mirerani wilayani Simanjiro mkoani Manyara wanatuhumiwa kuwafyatulia mabomu mawili ya machozi wachimbaji wadogo waliokuwa chini ya mgodi takribani Mita 240.


Wachimbaji hao Saba walikuwa mgodi namba P.M.L 0000049 Kitalu D unaomilikiwa na Theresia Wapalila walikumbwa na tukio hilo lisiloruhusiwa kisheria baada ya kutoboza eneo la Delta Kitalu C linachomilikiwa na Kampuni ya Tanzanite One.

Kutokana na tukio hilo baadhi ya wachimbaji kwenye mgodi huo walikamatwa na askari polisi na kufunguliwa taarifa ya kipoli kwa ajili ya kupatiwa matibabu kutoka Kituo cha Polisi Mirerani.

Wakizungumzia tukio hilo juzi Mirerani wachimbaji hao walidai kitendo cha kupigwa mabomu chini ya ardhi ikiwamo kuharibu mundombinu ya umeme, kunyang’anywa vifaa vya kazi kimewaathiri zaidi kisaikolojia pamoja na afya zao.

Wachimbaji waliokamatwa na kufikishwa kituo cha polisi kisha kupewa fomu ya matibabu ni Boxer Dennis (35), Phillipo Paul (31), Ramadhani Hamza, Hamis Hassan (30), Edmund Mosha, Benjamin Shakoti (47) na Emmanuel Afred (25)

Akizungumza kwa niaba yao Meneja wa Mgodi huo Frank Mushi alisema vitendo hivyo vya kupiga mabomu na kutembea na silaha za moto chini ya migodi vimekuwa vikifanywa na askari polisi wanaotumia na mwekezaji wa Tanzanite One.

Alisema siku ya kutekwa kwa wachimbaji hao askari hao polisi wakiwa na maofisa wa Tanzanite One walizama chini ya mgodi wakiwa na silaha za moto na mabomu ya machozi ambapo katika purukushani hiyo vijana wawili walinusurika na kuja kutoa taarifa.

“Hiki ni kilio kwetu pindi tunapotobozana wamekuwa wakitumia nguvu kubwa kinyume na sheria kwani wanatumia uporaji wa vifaa vya kazi. Tangu tumeanza kazi kwenye hii Shafti tulifikisha Mita 240  na tayari tulikuwa tumeanza kufanya uzalishaji.

“Tukarudishwa nyumba na kubaikiziwa Mita 30 kutoka kwenye sehemu tunayoiita kiraka ili tubadili muelekeo, tuliwaambia kwanii waturudishe mita zote hizo wakati inatakiwa kurudi Mita 10 au 15 nyuma,” alisema Mushi.
  
Akizungumzia tukio hilo Mkurugenzi mwenza wa Tanzanite One inayochimba kwa ubia na Serikali kupitia Shirika la STAMICO, Faisal Juma alisema, changamoto kubwa inayojitokeza ni kwa wachimbaji wadogo kushinda kutambua mipaka na kuheshimu sheria.

“Mgodi ule si wa kwetu pekee pale tunachimba kwa ubia na Serikali kupitia STAMICO. Hivyo ni lazima vyombo vya Dola viwepo ili kusimamia maslahi ya umma na kuona yakilindwa.

“Sasa kwa eneo la Delta ambalo hawa wanalalamika kuwa lilikuwa halichimbwi hiyo si sababu sasa hivi limeanza uzalishaji na linamilikiwa kisheria na Tanzanite One. Ni kweli wachimbaji wadogo katika harakati zao za kuchimba wanapitiliza na kuingia eneo hili.

“sisi na serikali kwa pamoja tunayo haki ya msingi ya kusimamia maeneo hayo yawe salama.Uamuzi unaochukuliwa mara nyingi ni wa kuwarudisha nyuma ambao umekuwa ukilenga usalama mgodini na kulinda maslahi ya serikali na mwekezaji,” alisema Juma.

Naye Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kaskazini Adam Juma akizungumzia kitendo hicho alisema kwamba licha ya sheria ya madini kutozungumizia suala mabomu chini ya ardhi bado wao kama Wiara hawaruhusu kufanyika kwa vitendo hivyo.

“Hatuhitaji kutumia nguvu kubwa ya kuwapiga Watanzania mabomu ya machozi chini ya ardhi kwasababu tu ya mtobozano wa uchimbaji suala hili linahitaji mazungumzo zaidi.

“Hata hao Tanzanite One tulishawapa maagizo ya maandishi kwamba hairhusiwi kutumia risasi za moto chini wala mabomu.Sisi tuna ofisi pale Mirerani wanatakiwa kwenda kutoa taarifa muda wowote na tumekuwa tukishawashauri kufanya mazungumzo badala ya kutumia nguvu.

Mwisho. 


No comments:

Post a Comment