Wednesday, May 31, 2017

UJERUMANI YATOA EURO MILIONI 2.9 UPEMBUZI YAKINIFU BARABARA YA ARUSHA-MARA


Na ELIYA MBONEA
-ARUSHA

SERIKALI ya Ujerumani kupitia Benki yake ya Maendeleo ya (KFW), imetoa kiasi cha Euro Milioni 2.9 kwa ajili ya shughuli za upembuzi yakinifu wa Barabara ya Arusha hadi Mara kupitia mkoani Simiyu.

Barabara hiyo inayotarajia kubadilisha maisha na uchumi wa wananchi sasa itapita katika maeneo ya wilaya  ya Karatu, Mbulu, Singida, Lalago, Kolandoto  mkoani Simiyu kisha kuingia Mara.


Ujenzi wa barabara hiyo uliopangwa awali kupita katikati ya Hifadhi ya Serengeti, lakini Mashirika na Asasi za kiraia duniani zinashughulika na mazingira zilipinga mradi huo zikidai utaathiri Ikolojia ya Hifadhi ya Serengeti.

Akizungumza wakati wa mkutano ulioshiikisha wadau kutoa maoni yao juu ya kuanza kwa upembuzi yakinifu Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mrisho Gambo aliwataka  wadau  kutoa  mapendekezo  makini yatakayolenga mambo  muhimu  ya kusaidia  mradi  kuwa  na  tija  kwa  wananchi  na  Taifa. 

“Tunaihitaji barabara,  pia uhifadhi ni muhimu na tunauhitaji. Lazima tuhakikishe mambo haya yote yanawekwa  bayana  na  kujadiliwa  kwa kina  ili  kuhakikisha mradi  unakuwapo  lakini  pia rasilimali  zinakuwa salama,” alisema Gambo 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Miradi ya Barabara kutoka Wakala wa Barabara nchini (TANROAD), Makao Makuu Crispin  Ako alisema,  kazi  ya  upembuzi huo  imeshaanza  na   inatarajiwa  kukamilika  ifikapo June Mwaka,  2018.

Nao baadhi ya wadau waliohudhuria majadiliano hayo akiwamo Mkuu wa wilaya ya Maswa inakopita barabara hiyo Dk. Seph  Shekalage alisema, ujenzi wa barabara hiyo utainua hali za kiuchumi za wananchi hao.

“Maeneo mengi ambako barabara hii itapita kuna fursa  nyingi  za  wananchi kuwekeza  na hatimaye kukuza kipato chao, huko kuna wakulima ambao kwa miaka mingi wamekuwa wakilima na mazao yao kushindwa kuyafikisha sokoni kwa wakati,” alisema Dk. Shekalage na kuongeza:

“Tunaamini fursa sasa zinakwenda kufunguka kwa wananchi wa maeneo hayo ili nao waweze kujiongezea kipato na kupata maendeleo kupitia barabara,” alisema.

Akiwa pia ni mtaalamu katika eneo la afya Dk. Shekalage alisema ujio wa barabara hiyo utakuwa pia muhimu na faida kubwa kwa wananchi walioteseka kwa miaka mingi kwa kushindwa kufika katika hospitali za kisasa kutokana na miundombinu mibovu.

Naye Mtaalamu wa masuala ya Uhifadhi Gerald  Bigurube  alionyesha kufurahishwa na barabara hiyo kupita kwenye mikoa ambayo haihusishi Hifadhi ya Seerengeti kama yalivyokuwa mapendekezo ya awali.

“Kwa sasa hakuna  eneo  litakaloharibu  uhifadhi  wala  kugusa  ikolojia  ya  viumbe  wengine wakiwemo  wanyamapori,” alisema Bigurube na kuongeza:

"Kubwa hapa ni maeneo kama ya wilaya ya Mbulu  ambayo  kwa  miaka mingi licha  ya  kuwa  na  fursa  kubwa  za  kilimo  bado maendeleo  yaliendelea kudororo kutokana  na  kukosa  miundombinu  bora  ikiwamo ya barabara,” alisema.


Mwisho. 

No comments:

Post a Comment