Wednesday, May 31, 2017

TANAPA YAPONGEZWA KUSAIDIA WAZAWA KUWEKEZA SERENGETI

Na JANETH MUSHI,
-ARUSHA

SHIRIKA la Hifadhi za Taifa  (Tanapa),limepongezwa kwa kuitikia wito na kuwasaidia wawekezaji wazawa   kuwekeza ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti,hatua iliyochangia kuongeza wigo wa kufanya biashara na kukuza utalii.


Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki na Mwenyekiti wa Umoja wa Waongoza Watalii Tanzania (Tato),Wilbard Chambulo,alipokuwa akizungumza katika maonyesho ya utalii ya 'Karibu Travel Market Fair',yaliyofanyika katika viwanja vya Magereza,vilivyopo eneo la Kisongo nje kidogo ya jiji la  Arusha.

Chambulo alisema kuwa Tanapa imewasaidia kuwekeza na kupanua wigo  kibiashara tofauti na miaka ya nyuma ambapo  hadi sasa kuna kambi za kitalii 138 katika hifadhi hiyo ambazo zote ni za wawekezaji wazawa.

"Serengeti tunafanya nao kazi vizuri kwelikweli ninafikiri watu wote wanafahamu hapa,Tanapa kwa ujumla nawapongeza kwa kuitikia wito na kutusaidia sisi hasa watanzania kuwekeza ndani ya hifadhi ya Serengeti,kule tuna kambi nyingi"alisema na kuongeza

"Unajua sisi waswahili unakuwa na Dola za Marekani 10,000 au 20,000 unanunua vihema vyako,unapiga kule unafanya biashara,hadi sasa biashara imepanuka leo kule Serengeti tuko 138 tumewekeza,hii ni habari nzuri tunaishukuru Tanapa na juhudi za serikali kwa ujumla,kwani imetuongezea wigo wa kufanya biashara,"

Kiongozi huyo aliwataka wadau wa utalii kuhakikisha wanafanya biashara zao kwa kuzingatia na kufuata kanuni na sheria ikiwa ni pamoja na kulipa kodi,kukata leseni na kuwa Umoja huo hautakuwa tayari kumtetea mfanyabiashara anayekiuka sheria au taratibu zilizowekwa.

Awali akizungumzia sekta ya utalii,Waziri wa Maliasili na Utalii,Prof Jumanne Maghembe,alitaja changamoto nyingine inayoikabili sekta hiyo ambalo inaendelea kuwa kubwa ni kuingizwa kwa idadi kubwa ya mifugo katika hifadhi hasa mifugo kutoka nchi jirani.

Alisema katika hifadhinza taifa hapa nchini mifugo mingi inayochungwa ndani ya hifadhi inatoka nchi za jirani,akitolea mfano upande wa Magharibi mwa Tanzania asilimia 68 ya ng'ombe waliopo kwenye hifadhi wanatoka kwenye nchi moja ambayo hakuitaja,huku asilimia 27 nyingine wakitoka kwenye nchi nyingine.

"Tumezidiwa na tatizo la kuchunga ng'ombe kwenye hifadhi,hili ni tatizo kubwa,mtalii hawezi kutoka Scotland anakuja kuona pundamilia badala yake anaona punda au ng'ombe huku kiingilio kwenye hifadhi kikiwa Dola za Marekani 200 halafu wanachoona ni ng'ombe,unajua siyo vizuri lazima tushirikiane tumalize tatizo hili,"alisema na kuongeza

"Lazima tujue kitu kimoja,hawa wenye mifugo siyo ya watu nje ya jamii yetu na lazima na wenyewe tushughulike nao vizuri.Siyo leta kiboko chapa ondoka,hapana lazima tulimalize kwa kushirikia na ndani ya kipindi cha mwaka mmoja na nusu ujao liwe limeisha,"

"Hao wafugaji wa nje wanaona hapa kwetu tuna ardhi ni shamba la bibi,kwa hiyo hii hatuwezi kuvumilia hawa lazima waondoke,hivyo lazima tufikirie namna ya kushughulika na wa kwetu wanaobaki,maana na wenyewe iko shida,na kuangalia namna ya kusaidia mahitaji ya watu wenye mifugo lakini hawana mahali pa kuchunga,"alisema Profesa

Kuhusu ujangili alisema serikali inapambana na tatizo hilo kwa kiasi kikubwa na kuwa hadi sasa watuhumiwa  966 bado kesi zao zinaendelea,huku katika kipindi cha mwaka 2016-2017 walihukumiwa zaidi ya watu 276 na  vifungo vyao vikiwa kati ya  miaka 12 hadi 30 na wengine kifungo na wakitoka walipe faini ya Dola za Marekani Milioni 54.

Mwisho


No comments:

Post a Comment