Tuesday, January 2, 2018

TAWA YAWAHAMISHA NYOKA, PIMBI, MIJUSI IKULU YA CHAMWINO

MAMLAKA ya Usimamizi wa Wanyamapori nchini (TAWA), imefanikisha zoezi la kuhamisha wanyamapori katika maeneo ya makazi ya viongozi wa kitaifa ikiwamo Ikulu ya Chamwino Dodoma inayoendelea kukarabatiwa.

Kuhamishwa wanyamapori hao kulianza Mei hadi Agosti mwaka huu kukihusisha Pimbi zaidi ya 300, Nyoka zaidi ya 50, Kenge na Mijusi ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii.

Hayo yalibainishwa na Meneja wa Pori la Akiba la Swaga Swaga lililopo wilaya ya Chemba na Kondoa, Alex Choya alipokuwa akijibu maswali ya wanahabari waliotembelea pori hilo ili kujionea vivutio na changamoto.

Meneja Choya


Akijibu maswali Meneja Choya alisema, pori hilo lililoanzishwa mwaka 1997 lina Kilomita za mraba 871 lina vivutio vingi vya utalii wa upigaji picha na uwindaji, huku wanyama Simba, Tembo, Tandara wakubwa na wadogo wakipatikana.

Alisema TAWA inayosimamia wanyamapori nchini hivi karibuni ilipokea ilipokea agizo la kuhamisha wanyapori katika makazi ya viongozi wa kitaifa yanayofanyiwa ukarabati ikiwamo Ikulu ya Chamwino na makazi ya Waziri Mkuu Dodoma.

“Wizara ya Maliasili na Utalii ilipokea agizo la kuhamisha viumbe hai wakiwamo Nyoka zaidi ya 50, Kenge, pimbi zaidi ya 300 na mijusi kutoka makazi makuu Ikulu ya Rais Chamwino Dodoma na Waziri Mkuu.

“Zoezi la kuwahamisha na kuwaleta Pori la Akiba la Swaga Swaga lililopo karibu lilifanyika kwa ufanisi. Na aina mojawapo ya nyoka waliohamishwa ni Swila na Vifutu,” alisema Choya na kuongeza:

“Wanyamapori hao walikuwa wakiishi kwenye makazi yao ya asili yenye majabali, miamba na misitu mikavu ambayo nyoka hupendelea na wakati mwingine hata kwenye makazi ya watu kwasababu nao ni viumbe hai kama sisi,” alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TAWA Dk, James Wakibara akizungumzia ufanisi wa zoezi hilo alisema, zoezi la kuhamisha wanyamapori la kawaida kufanyika kulingana na mahitaji ya eneo husika na aina ya wanyamapori waliopo.

“Tulipoambiwa kuwahamisha wanyamapori kuwatoa Dodoma na kuwaleta huku Swaga Swaga kilikuwa ni kitu kidogo na cha kawaida,” alisema Dk. Wakibara na kuongeza:

Dk.Wakibara

“Tunajivunia kutoa huduma hiyo kwa Makao Makuu yetu ya nchi Dodoma. Lakini pia imezidi kutututambulisha TAWA ni shirika kubwa katika uhifadhi wanyamapori,” alisema.

Naye Kaimu Mkurugenzi anayesimamia huduma za usimamizi wa wanyamapori TAWA David Kanyata zoezi hilo lilifanyika kwa ufanisi mkubwa kutokana na kazi hiyo kuwa sehemu ya majukumu waliyokabidhiwa.

Kupelekwa kwa wanyamapori hao katika Pori la Akiba la Swaga Swaga kumekuwa ni sehemu ya maandalizi ya kuhamia kwa viongozi wa kitaifa katika makao makuu ya nchi Dodoma.

Tayari Waziri Mkuu Kassimu Majaliwa alishamia Dodoma ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais Dk. John Magufuli kuhakikisha viongozi wote wa kitaifa wanahamia makao makuu ya nchi.

Mbali ya Waziri Mkuu tayari Makamu wa Rais Mama Samia Hassan Suluhu naye amehamia kwenye makazi yake mjini humo hivi karibuni huku Rais Dk. Magufuli akitarajiwa kuhamia mjini Dodoma mwakani.


Mwisho. 

No comments:

Post a Comment