Tuesday, June 13, 2017

JIJI LA ARUSHA LANG’AA KIDATO CHA TANO

Na MWANDISHI WETU
-ARUSHA


HALMASHAURI ya Jiji la Arusha imefanikiwa kupeleka wanafunzi 578 Kidato cha tano kutoka katika Shule zake za Sekondari 23.

Jiji la Arusha lipo Kaskazini mwa Tanzania likiwa ndio kioo cha sekta ya utalii na kituo cha biashara ya madini ya Tanzanite yanayochimbwa Mirerani, Simanjiro mkoani Manyara.


Akielezea kuhusu mafanikio ya kupeleka wanafunzi wengi Kidato cha Tano, Mkurugenzi Mtendaji wa Jiji la Arusha Athuman Kihamia amewataka walimu kuongeza bidii ya kufundisha na kutobweteka kwa matokeo ya sasa.

“Niwaombe walimu waongeze bidii ili uwekezaji unaofanywa na serikali uakisiwe katika ufaulu wa watoto, nisisitize pia kwa wazazi na walezi waendelee kutoa ushirikiano kwa walimu ili kusukuma mbele gurudumu hili la elimu kwa watoto wetu.

Nao baadhi ya wazazi waliobahatika kuzungumzia matokeo hayo wameishukuru serikali kwa kuendelea kuhakikisha elimu bora inatolewa kwa watoto wao.

“Tunamshukuru Rais Dk. John Magufuli kwa sera yake ya elimu bure hakika imekuwa nguzo kwetu sisi wazazi. Lakini pia kupitia wasaidizi wake Mkuu wa Mkoa Mrisho Gambo, Mkuu wa wilaya Fabian Daqqaro na Mkurugenzi wa Jiji Kihamia,” alisema Mzazi Johari Lyimo mwenye mtoto katika Shule ya Sekondari Kaloleni jijini hapa.

Kwa miaka mingi sas Jiji la Arusha limekabiliwa na changamoto katika sekta ya elimu, hatua ambayo serikali kupitia kwa Mkurugenzi wa Jiji imeendelea kutoa majawabu kwa changamoto mbalimbali.

Baadhi ya changamoto zinazotajwa kutatuliwa ili kufikia matokeo bora ni pamoja na kulipa madeni ya walimu kupitia mapato ya ndani, kuongeza vyumba vya madarasa 147 kwa Shule ya Msingi na Sekondari.

Nyingine ni ukarabati wa vyumba 27 vya madarasa kwa kipindi cha miaka miwili na kuhakikisha kila Shule ya Sekondari inakuwa na  maabara yenye vifaa vyote.



No comments:

Post a Comment