Thursday, January 31, 2013

RUSHWA YA MILIONI 2 YAMPONZA MWANDISHI WA HABARI ARUSHA



*Apandishwa kizimbani, akosa dhamana apelekwa gerezani

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoani Arusha imempandisha kizimbani Mwandishi wa habari wa kujitegemea  Joseph Ngilisho kwa tuhuma za kuomba rushwa ya Sh. Milioni 2.

Mwendesha Mashitaka wa TAKUKURU Rehema Mteta alidai juzi mbele ya Hakimu Mkazi Hawa Mguruta wa Mahakama ya Arusha kuwa Ngilisho anatuhumiwa na makosa matatu, kuomba, kushawishi na kupokea Sh. 500,000 kati ya Sh. Milini 2 alizoomba.

Mteta alida kwamba mtuhumiwa huyo anadaiwa kutenda makosa hayo katika siku tofauti akiwa jijini Arusha.

Mwendesha Mashitaka Mteta alifafanua kwamba Januari 12, Mwaka huu, Ngilisho anadaiwa kuomba Sh. Milioni 2 kutoka Ofisa Mwandamizi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) Phil Kleruu ili asiandike vibaya habari zake ndani ya Gazeti la Dira.

“Shitaka la pili anadaiwa kulitenda Januari 25 Mwaka huu, ambapo aliomba rushwa kutoka kwa ofisa huyo ili aandike habari za kumsafisha gazetini.

“Januari 28, Mwaka huu, mtuhumiwa alikamatwa akipokea Sh. 500,000 ikiwa ni sehemu ya malipo ya Sh. Milioni 2 alizoomba,” alisema Mteta.

Kwa upande wake akitakiwa kuthibitisha madai hayo mshitakiwa  Ngilisho anayewakilishwa na Wakili Edmund Ngelemi,  alipinga madai hayo.

Akitoa nafasi ya dhamana kwa mtuhumiwa Hakimu Mguruta alisema mshitakiwa anatakiwa kuwa na wadhamini watatu huku mmoja kati yao akiwa ni mtumishi wa serikali.

Pamoja na kupatikana kwa wadhamini hao bado Hakimu alikataa nyaraka zao kwa madai zilikuwa hazijajitosheleza kisheria,hatua iliyomsababishia mtuhumiwa kupelekwa mahabusu katika gereza la Kisongo hadi hapo taarifa zitakapokuwa zimekamilika

Kesi hiyo imeahirishwa hadi  Februari 12, Mwaka huu itakapotajwa tena.

Habari kutoka eneo la tukio alikokamatwa mwandishi huyo zilidai kwamba mara baada ya kupokea fedha hizo aliwashtukia maofisa wa TAKUKURU wakimzunguka ndipo alikimbia.

Habari hizo ziliendelea kubainisha kuwa mbio za mwandishi huyo hazikufua dafu kutokana na kukimbia kuliko sababisha kuchana suruali yake, na kujikuta akiingia akiingia ndani ya ofisi za Usalama wa Taifa zilizopo jirani na Hoteli ya East Africa.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment